Home » » Nahodha Matatani,,,,,,

Nahodha Matatani,,,,,,

Written By Koka Albert on Sunday, April 15, 2012 | 11:58 PM

KAMATI YA LOWASSA YAMCHUNGUZA KWA MADAI YA KUKWAMISHA KILIMO KWANZA, MWENYEWE ASHANGAA Daniel Mjema, Dodoma
KAMATI ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, inayoongozwa na Edward Lowassa imependekeza kuundwa kwa kamati teule ya watu wanne kumchunguza Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Shamsi Vuai Nahodha kwa madai ya kukataa kutekeleza agizo lake lililotaka nusu ya matrekta ya Kilimo Kwanza yaliyopelekwa Shirika la Uzalishaji Mali la Suma JKT, yapelekwe Magereza.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Lowassa alithibitisha kuundwa kwa kamati hiyo ndogo lakini akasema haina madaraka mpaka Spika, Anne Makinda, atakaporidhia.

“Ni kweli tumependekeza kuundwa kwa kamati ndogo kuchunguza jambo hilo na tumempelekea Spika, lakini kwa sasa haina madaraka yoyote mpaka Spika atakaporidhia kuundwa kwake na kuitangaza,” alisema Lowassa.

Spika wa Bunge Anne Makinda hakupatikana jana kuzungumzia suala hilo baada ya simu yake ya mkononi kutopatikana mara kadhaa.

Naibu Spika, Job Ndugai, alisema kama mapendekezo hayo yapo, basi yamepelekwa moja kwa moja kwa Spika… “Ninafahamu kulikuwa na maagizo kuhusu hilo jambo, lakini kama imefika hadi kuunda kamati mimi sifahamu kwa sababu hayo mapendekezo yatakuwa yamekwenda moja kwa moja kwa Spika,” alisema Ndugai.

Chanzo cha habari kutoka bungeni kimeitaja kamati iliyopendekezwa kumchunguza Waziri Nahodha kuwa itawajumuisha Brigedia Jenerali mstaafu, Hassan Ngwilizi, Masoud Salim Abdallah, Hilda Ngoye na Muhammed Seif Khatib.

Msingi wa pendekezo la kamati hiyo unatokana na Jeshi la Magereza kuwa na nguvu kazi ya kuzalisha tofauti na Suma JKT, hali ambayo ingesaidia kuondoa utegemezi wa chakula kwa wafungwa.

Hata hivyo, inadaiwa kwamba Waziri Nahodha alikataa kutekeleza agizo hilo na alipoitwa tena kwenye kamati ili kueleza sababu zake, anadaiwa kujibu kuwa Magereza hawahitaji matrekta hayo kwa sababu hayana ubora.

Alisema majibu hayo yalionekana kuishtua kamati hiyo hasa ikizingatiwa kuwa Nahodha ni Mjumbe wa Baraza la Mawaziri, ambaye alishiriki kupitisha mpango wa kuagizwa kwa matrekta hayo.

“Majibu yake yalionekana kuwa kuna kitu kimejificha nyuma kwa sababu yeye alishiriki kupitisha mpango wa kuagizwa matrekta hayo na alikuwa na fursa ya kulishauri Baraza la Mawaziri lisiendelee na mradi huo kama ni mbovu kama anavyoeleza,” kilieleza chanzo hicho cha habari.

Chini ya mpango huo wa Serikali wenye lengo la kuleta mapinduzi katika sekta ya kilimo, matrekta 1,860 ya Farm Track kutoka India yameingizwa nchini ikiwa ni mkopo wa Dola 40 milioni za Marekani.

Kutokana na Kamati ya Lowassa kutilia shaka majibu ya Waziri Nahodha, kamati hiyo iliwaita makamishna wa Jeshi la Magereza ambao wanadaiwa kutamka kuwa wanayahitaji, lakini kikwazo ni waziri wao.

“Kamati iliambiwa Waziri ndiye hataki matrekta hayo kwa sababu anazozijua yeye na hii ndiyo iliwafanya wajumbe wa kamati kupendekeza iundwe kamati ndogo kuchunguza sakata zima,” kilidai chanzo hicho.

Msimamo wa Nahodha
Alipoulizwa kuhusu madai hayo jana, Waziri Nahodha alikiri kushauriwa na Kamati ya Bunge kuhusu suala la kupeleka matrekta Magereza lakini akasema: "Sasa haiwezekani kwa kuwa matrekta yenyewe hayapo."

Alisema kamati hiyo ya Bunge ilimtaka apeleke matrekta 72 Magereza kwa ajili ya kutekeleza Kilimo Kwanza lakini akasema hilo linahitaji upatikanaji wa fedha.

"Kwanza sina taarifa kwamba hapa kuna mgogoro unaoweza kufikia kiwango hicho cha (kuundiwa tume) kwa kuwa kamati yenyewe inajua kwamba matrekta yenyewe hayapo.

Hatuna fedha sasa za kuyanunua leo. Tunategemea fedha zenyewe zipatikane baada ya Bajeti ya mwaka huu 2012/2013," alisema Waziri Nahodha na kuongeza:

"Kilichotokea ni kwamba kamati imeishauri wizara yangu inunue matrekta hayo 72 na mimi nimewashauri wao waende wakayaangalie kwanza halafu watushauri ili tukifanya uamuzi uwe wa busara."

Waziri Nahodha alisema kimsingi wizara yake iko mstari wa mbele kutekeleza Kilimo Kwanza na inajipanga kwa hali na mali kuliwezesha Jeshi la Magereza lijitegemee kwa chakula na hata ikiwezekana lianze kuuza chakula hicho.

“Tumepokea ushauri wa kamati na ni mzuri na hivi sasa tunatafuta pesa ili tuyanunue matrekta hayo kwa ajili ya Kilimo Kwanza. Ushauri wa Kamati ni mzuri mno kwa sababu utatusaidia kuzalisha chakula kwa wingi ili tuwalishe wafungwa na kuuza cha ziada. Tuna lengo la kujitegemea."

Hivi karibuni, Serikali ya India ilisema inajipanga ili kuwekeza zaidi Tanzania, kutokana na mafanikio yaliyopatikana katika miradi mbalimbali ya ushirikiano kati ya nchi hizo ukiwamo huo wa matrekta.

Ahadi hiyo ilitolewa na Kaimu Balozi wa India nchini, Hemalata Bhagirath alipotembelea mradi wa matrekta hayo eneo la Mwenge, Dar es Salaam na kuridhishwa na mafanikio yake.

Alisema lengo la kuletwa nchini matrekta hayo ni kukopeshwa wakulima wa Tanzania ili kufanya mapinduzi ya kilimo kupitia mpango wa Kilimo Kwanza.

Balozi Bagirathi alisema kutokana na mwitikio mzuri kwa Watanzania kwa matrekta hayo, nchi yake inaweza kuangalia uwezekano wa kufungua kiwanda cha matrekta hayo ili kutosheleza mahitaji ya Kilimo Kwanza.
Share this article :

Post a Comment

KARIBU KATIKA WEBSITE YA KIJANJA, KUPATA HABARI MBALIMBALI ZA NDANI NA NJE YA NCHI. PIA UTAPATA MAMBO YA ACADEMIC. KARIBU SANA
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. GetInformedTz - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger