Home » » CCM sasa vurugu tupu

CCM sasa vurugu tupu

Written By Koka Albert on Thursday, May 31, 2012 | 12:35 AM

MUKAMA ASEMA KINA MPASUKO MKUBWA KAMA G8, NATO, MAIGE AMLIPUA NAPE, ASEMA NI GAMBA LINALOPASWA KUVULIWA
Amini Yasini, Rufiji na Ahmed Makongo, Kahama
HALI ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), si shwari na Katibu Mkuu wake, Wilson Mukama amekiri kwamba hivi sasa kina mpasuko mkubwa unaotokana na makundi yanayofanana na yale ya Umoja wa Kujihami wa Nchi za Magharibi (Nato) na Umoja wa Mataifa yenye nguvu kubwa kiuchumi duniani (G8).

Wakati mtendaji mkuu huyo wa chama tawala akitoa kauli hiyo, aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige ameibuka na kumshambulia waziwazi, Katibu wa Taifa wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye akimtuhumu kukiharibu kwa utendaji mbovu, hivyo kutaka ang’olewe haraka akidai kuwa ni gamba.

Nchi zinazounda G8 ni Marekani, Canada, Ufaransa, Ujerumani, Italia, Japan, Russia na Uingereza ambazo pia baadhi yao, ndizo zinazounda Nato, umoja wenye wanachama 28.

Mukama alitoa kauli hiyo juzi wilayani Rufiji wakati akizungumza na umati wa wananchi na wanachama wa chama hicho waliofurika katika Viwanja vya Corecu, Kata ya Kibiti.

Alisema baadhi ya wanachama wa CCM wamekuwa ni wasaka madaraka na wanapokosa huamua kuunda makundi ya uhasama ambayo hawataki kuyavunja pindi mchakato wa kutafuta mgombea unapomalizika.

“Makundi yaliyoundwa tangu 2005 na 2010 yanaendelea kukitafuna chama, wanachama wakinyimwa uongozi wanaanza uhasama, hatufiki malizeni makundi,” alisema.

Alisema makundi hayo pia yako katika Wilaya za Mkuranga na Rufiji, ambako katika ziara yake amebaini mpasuko mkubwa unaotokana na fitina na uhasama miongoni mwa wapenzi na makada wa CCM na kusisitiza kwamba hayafai na ni hatari kwa mustakabali wa chama hicho kikongwe barani Afrika.

“Nikiwa Mkuranga nilitaarifiwa kuwa kuna makundi ya Nato na G8 na sasa nimefika Rufiji nimeyakuta makundi hayo. Jamani makundi hayo ya nini?”
Mukama ambaye aliwahi kushika nafasi mbalimbali za kiutendaji zikiwemo za Ukuu wa Wilaya ya Mafia akimrithi mtangulizi wake Hemedi Mkali, alisema aliwahi kugombea ubunge wa viti vya Taifa kupitia Juwata (iliyokuwa Jumuiya ya Wafanyakazi Tanzania), na aliposhindwa alikubali matokeo.

Alisema Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kusema bila CCM imara nchi yetu itayumba, akimaanisha kuwa hakuna chama mbadala cha kuongoza nchi zaidi yake.

Alitoa mfano wa Chama cha Democrat cha Marekani kwamba wanachama wake hawana kadi, bali mapenzi ya chama yako mioyoni mwao na wanapojiunga hawafanyi hivyo kwa lengo la kusaka madaraka... “Hii ni tofauti kubwa na nchi zetu ambako mtu akijiunga na chama kitu kwanza kufikiria ni kusaka madaraka,” alisema.

Alisema chama hicho kina mkakati madhubuti wa kupambana na watu wachache wanaotaka kukimiliki wakitumia nguvu ya fedha.

Alisema baadhi ya wanachama wa kawaida wamejiona kuwa hawana nafasi katika chama chao wakiamini kuwa kimetekwa na wenye fedha na kuongeza kwamba mwanachama wa kawaida hawezi kuongoza bila rushwa.

“Hapana! Chama chetu hakitakubali hali hiyo. Ni hatari sana kwa mustakabali wa chama chetu na nchi yetu,” alisema na kuongeza kuwa wanachama wa kawaida wanatakiwa kugombea hata kama hawana fedha.

Alisema chama kipo katika uchaguzi wake wa ndani na kuwataka wanachama kufanya uamuzi sahihi wa kuchagua viongozi waadilifu wasiotumia rushwa, kwani kufanya hivyo kunaweza kusababisha kuingia watu katika uongozi waliotoa rushwa.

Katika mikutano yake hiyo, Mukama alitamba kuwa chama chake hakitishwi na wapita njia akimaanisha wapinzani wanaodai kuwa hakijafanya kitu.

Alisema CCM ni chama makini na sikivu katika kusikiliza kero za wananchi akitamba kwamba kimejenga Daraja la Mkapa ambalo limekuwa kiunganishi kati ya Mikoa ya Lindi, Mtwara na Dar es Salaam na umeme wa gesi unaotoka kusini ambao wananchi wa Rufiji wananufaika nao kwa sasa.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Rufiji, Mrisho Matimbwa alisema katika uchaguzi uliopita wa chama hicho kulikuwa na makundi mawili, ya Bush na Al Qaeda ambayo kwa sasa yamekufa na kubakia mpasuko katika halmashauri kuu ambako aliahidi kuutatua.

Maige na Nape

Akizindua matawi mawili ya wakereketwa wajasiriamali wa CCM katika Kijiji cha Isaka, Kahama, Shinyanga, Maige ambaye ni Mbunge wa Msalala alimtaka Nape kuacha tabia yake ya kutoa kauli ambazo kwa namna moja au nyingine zinaelekea kukidhoofisha chama.

Alimtaka kupima utendaji wake tangu alipoishika nafasi hiyo ya Itikadi na Uenezi na kujiuliza ni wanachama wangapi wameingia ndani ya chama hicho.

Alisema sasa hivi kuna wimbi kubwa la wanachama wa chama hicho kuhama na kukimbilia upinzani na kusema ni wajibu wa Nape kupima na kuona kuwa kazi ya itikadi na uenezi haiwezi na kwani hajui wajibu wake akisema ni mtu wa kumhurumia.

Maige alisema mbali ya kushindwa kuzuia wimbi la wanachama kukihama CCM pia hapaswi kuvumiliwa kutokana na kauli yake kwamba hata kama wanachama watahama wote na akabaki yeye (Nape) peke yake, haitakufa. Alisema kauli hiyo haikijengi chama, bali kuchochea makundi ambayo yanaweza kukibomoa.

Alisema akiwa mwana CCM anaona kwamba sasa hivi Nape amekuwa hafanyi kazi ya uenezi na kukirejeshea haiba na mvuto ambao umepotea kwa wananchi na kwamba, kazi anayoifanya sasa ni kukuza makundi na kusema ovyo.

Aliendelea kumshambulia Nape kwa maneno akisema amejenga jeuri, kiburi, dharau na ulevi wa madaraka huku akidai kwamba kitendo cha CCM kupoteza wanachama zaidi ya 10,000 kwa wakati mmoja mkoani Arusha na sehemu nyingine wanachama 3,000 ni ishara ya hatari lakini, Nape amekuwa akiwaita wanaohama kwamba ni mzigo.

“Huyu Nape ni lazima atupishe. amekifanya chama kama mali yake, yeye ndiye mwenye jukumu la kueneza sera za chama na kutafuta wanachama wapya, lakini ndiyo kwanza anasema waachwe waondoke, Chadema wanatamba kila siku yeye hajali, huyu nasema ni gamba ni bora atupishe,” alisema.

Baada ya mashambulizi hayo, Maige alijitetea kwamba maneno yake dhidi ya Nape yasitafsiriwe kama ni kuulilia uwaziri: “Ni uchungu nilionao kwa chama changu kuona kila siku zinavyokwenda ndivyo tunavyopoteza idadi kubwa ya wanachama, tuliyemkabidhi jukumu la uenezi anasema hajali, sasa huyu si atupishe mapema kabla mambo hayajaharibika?”
Share this article :

Post a Comment

KARIBU KATIKA WEBSITE YA KIJANJA, KUPATA HABARI MBALIMBALI ZA NDANI NA NJE YA NCHI. PIA UTAPATA MAMBO YA ACADEMIC. KARIBU SANA
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. GetInformedTz - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger