Home » » Necta yapunguzia adhabu wanafunzi 3,000

Necta yapunguzia adhabu wanafunzi 3,000

Written By Koka Albert on Wednesday, May 2, 2012 | 4:42 AM

Leon Bahati
BARAZA la Mitihani Tanzania (Necta), limepunguza adhabu ya kufutiwa matokeo watahiniwa 3,303 wa kidato cha nne mwaka 2011, waliobainika kufanya udanganyifu na kufungiwa kufanya mtihani kwa miaka mitatu, sasa watatumikia kifungo hicho kwa mwaka mmoja.

Tamko la Necta limekuja wiki chache baada ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kuwaahidi wabunge kuwa Serikali itawasiliana na baraza hilo na kuangalia uwezekano wa kupunguza adhabu hiyo.

Pinda alisema hayo kwenye kipindi cha maswali ya papo kwa papo baada ya Mbunge wa Mbozi Mashariki, Godfrey Zambi (CCM), kuitaka Serikali iwasamehe wanafunzi hao ambao aliwaelezea kuwa kitendo cha kuwafutia matokeo kilitosha kabisa na sasa waruhusiwe kurudia mtihani.

Katibu Mtendaji wa Necta, Dk Joyce Ndalichako, alisema jana kuwa baraza limechukua hatua hiyo baada ya kutathmini maombi mbalimbali yaliyotolewa na wakuu wa shule, wanafunzi waliofutiwa matokeo, wazazi wao na wadau wengine.

Hata hivyo, Dk Ndalichako hakueleza iwapo hatua hiyo wameichukua baada ya shinikizo la Serikali.
“Wadau wengi walikiri kosa, lakini waliomba kupunguzwa kwa adhabu ya kutofanya mitihani kwa miaka mitatu… Wakuu wa shule na watahiniwa husika wameahidi kuwa iwapo watapewa fursa hiyo watakuwa makini zaidi kuhakikisha wanazingatia taratibu za mitihani,” alisema Dk Ndalichako.

Kwa sababu hiyo, Dk Ndalichako alisema Necta imewaruhusu wafanye mtihani kama watahiniwa wa kujitegemea mwaka 2013, kwa sababu mwaka huu wameshachelewa katika mchakato wa usajili.

“Uamuzi wa Baraza umezingatia kuwa kitendo cha watahiniwa na wadau wengine walioathirika na adhabu hiyo kuomba msamaha kimeonyesha kuwa wametambua athari zinazoweza kutokea kutokana na kufanya udanganyifu,” alisema.

Necta ilitoa adhabu hiyo kwa wanafunzi hao wa kidato cha nne mwaka 2011, baada ya kufanya kikao Februari mwaka huu na kuthibitisha kuwa walifanya udanganyifu kwenye mitihani mbalimbali waliyofanya.
Licha ya kutoa msamaha, Dk Ndalichako alisema Necta itaendelea kutoa adhabu kali kwa wale ambao itabaini wamefanya udanganyifu kwenye mitihani.

Alisema bado Necta itaendelea kufanyia uchunguzi ripoti ya kamati maalumu iliyochunguza chanzo cha udanganyifu kwenye mitihani na wahusika wote watachukuliwa hatua.

Dk Ndalichako alisema matokeo ya awali ya uchunguzi huo yanaonyesha kuwa, kuna walimu na wasimamizi wa mitihani walioshirikiana kusababisha udanganyifu huo ikiwamo kuwafanyia mitihani.

“Watahiniwa wengine walichelewa kuingia katika vyumba vya mitihani wakisubiri uwezekano wa kupata taarifa za maswali ya mitihani kutoka kwa wasimamizi wasio waadilifu, kuyajibu na kuingia wakiwa tayari na majibu hayo,” alisema Dk Ndalichako.

Kasoro nyingine, ni baadhi ya wasimamizi kupangiwa shule wanazofundisha, wanafunzi kutofanyiwa upekuzi kabla ya mitihani, wanafunzi kusongamana na kutoa mwanya wa kutazamiana, wasimamizi na askari kusafiri kwenda kuchukua mitihani badala ya kupelekewa vituoni na mitihani kufunguliwa ofisini badala ya chumba cha watahiniwa.
Share this article :

Post a Comment

KARIBU KATIKA WEBSITE YA KIJANJA, KUPATA HABARI MBALIMBALI ZA NDANI NA NJE YA NCHI. PIA UTAPATA MAMBO YA ACADEMIC. KARIBU SANA
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. GetInformedTz - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger