Home » » Mwanasheria afafanua wasioapishwa kupata uwaziri

Mwanasheria afafanua wasioapishwa kupata uwaziri

Written By Koka Albert on Tuesday, May 8, 2012 | 2:23 AM


Patricia Kimelemeta
MWANASHERIA Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema, amesema Rais Jakaya Kikwete hajavunja sheria kwa kuwaapisha wabunge wateule kuwa mawaziri kabla ya kiapo cha Bunge.
Kauli hiyo imekuja siku chache baada ya baadhi ya wananchi kudai kuwa, Rais Kikwete alivunja sheria baada ya kuwateua wabunge na kuwaingiza kwenye baraza la mawaziri kabla ya kuapishwa bungeni.

Taarifa iliyotolewa na Jaji Welema ilieleza kuwa kitendo cha rais kuteua wabunge hao ni sahihi na kwamba wameahidi kutoa elimu kwa umma kuhusu Mamlaka ya Rais ya uteuzi wa Wabunge  kwa sababu ni jambo lenye maslahi ya jamii na linalohitaji kufafanuliwa.

“Msingi wa Katiba tunaoanza nao ni maelekezo ya masharti yaliyomo kwenye Ibara ya 55(4) kwamba. “Mawaziri na Naibu Mawaziri wote watateuliwa kutoka     miongoni mwa Wabunge”, ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

Ilifafanua kuwa Mamlaka ya Rais ya uteuzi wa Wabunge aliyopewa na masharti ya Ibara ya 66(1)(e) yenye aina ya Wabunge wasiozidi 10 watakaoteuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watu wenye sifa zilizotajwa katika aya za (a) na (c) za ibara ya 67 na angalau Wabunge watano kati yao wakiwa wanawake.  Wabunge aliowateua Mheshimiwa Rais wanatokana na Ibara hii.

Ilibainisha kuwa baada ya hatua zote hizi ikumbukwe kwamba aliyeteuliwa au kuchaguliwa kuwa mbunge anakuwa mbunge ama baada ya kutangazwa na Msimamizi wa Uchaguzi, au baada ya kuteuliwa na Tume ya Uchaguzi kwa wale wabunge wa viti maalumu au anapochaguliwa na Baraza la Wawakilishi au anapoteuliwa na Rais akitumia mamlaka yake ya uteuzi yanayotokana na Ibara ya 66(1)(e).

Ilieleza kuwa hivyo wabunge wanaohusika hawahitaji kuapishwa kwanza bungeni ili wawe wabunge na kwamba kiapo cha mbunge bungeni kinamuwezesha tu kushiriki katika shughuli za Bunge.

Ilifafanua kuwa katiba ya nchi haiweki kwa Rais masharti kwamba kabla ya kumteua mbunge wa aina hiyo kuwa Waziri au Naibu Waziri Mbunge huyo awe ameapishwa Bungeni kwanza na kwamba masharti mawili muhimu na ya kuzingatia ni kwamba mteule wa nafasi ya uwaziri au Naibu Waziri hatashika madaraka yake ila mpaka kwa mujibu wa Ibara ya 56 ya Katiba, awe ameapa kwanza mbele ya Rais kiapo cha uaminifu na pia kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi yake kitakachowekwa kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Bunge.

‘’Serikali inasisitiza kwamba wabunge ambao hawajaapishwa ndani ya Bunge ni wabunge na wanapoteuliwa kushika nafasi ya uwaziri au Naibu Waziri ni halali kwa kuwa uteuzi huo haukiuki masharti yoyote ya kikatiba au sheria’’ alisema
Share this article :

Post a Comment

KARIBU KATIKA WEBSITE YA KIJANJA, KUPATA HABARI MBALIMBALI ZA NDANI NA NJE YA NCHI. PIA UTAPATA MAMBO YA ACADEMIC. KARIBU SANA
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. GetInformedTz - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger