Home » » Wabunge waagiza jenereta kwa mkurugenzi wa Tanesco lizimwe

Wabunge waagiza jenereta kwa mkurugenzi wa Tanesco lizimwe

Written By Koka Albert on Tuesday, March 27, 2012 | 2:45 AM

KAMATI ya Hesabu za Mashirika ya Umma(POAC), imeagiza Bodi ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuondoa jenereta la dharura lililopo nyumbani kwa Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, William Mhando kuanzia leo ili naye ajue machungu ya kukatika umeme mara kwa mara.

Wakati POAC ikiagiza kuondolewa kwa jenereta hilo, taarifa zinaeleza kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Tanesco, Jenerali Mstaafu, Robert Mboma amemwandikia Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja akihoji sababu za kutokutekelezwa kwa agizo la Rais Jakaya Kikwete la kulipatia shirika hilo kiasi cha Sh408 bilioni kwa ajili ya kujiendesha.
Barua ya Mboma ya Machi 20, mwaka huu kwenda kwa Ngeleja, ambayo gazeti hili imefanikiwa kuiona, ilisema mnamo Machi, 8 mwaka huu, Rais Kikwete aliagiza Tanesco ipewe haraka mkopo huo wa Sh408 bilioni lakini akasema hadi sasa amri hiyo ya Amiri Jeshi Mkuu haijatimizwa.

“Mheshimiwa Rais tarehe 8 Machi aliagiza kuwa mkopo huo wa Sh408 bilioni upatikane haraka. Lakini, sisi tunazunguka na hivyo kushindwa kutii amri ya Amiri Jeshi Mkuu wa Tanzania. Katika hali ya kawaida, tunatakiwa tufanyekazi usiku na mchana kwa nia ya kukamilisha maagizo halali ya Rais wa Jamhuri ya Muungano," inasema sehemu ya barua hiyo ya Mboma.

Katika sehemu nyingine ya barua hiyo, Mboma alisisitiza: "Hali ya mabwawa yanayotegemewa ya Mtera na Nyumba ya Mungu ni mbaya sana. Ukosefu wa mafuta utatulazimu tutumie maji hayo... hii maana yake ni kuwa mwakani tutalazimika kukodi mitambo mingine ya dharura kwa sababu mitambo ya sasa, muda wake utakuwa umekwisha. Watanzania hawatatuelewa na Tanesco italaumiwa bure kwa sababu tuko ambao hatutii amri za ngazi za juu."

Mboma katika kuhakikisha agizo hilo la Rais linatekelezwa, aliomba kikao kati yake na Waziri Ngeleja, Katibu Mkuu wa Nishati na Madini, wajumbe wawili wa bodi, menejimenti ya shirika hilo na wajumbe wengine ambao waziri huyo angeona wanafaa.
Share this article :

Post a Comment

KARIBU KATIKA WEBSITE YA KIJANJA, KUPATA HABARI MBALIMBALI ZA NDANI NA NJE YA NCHI. PIA UTAPATA MAMBO YA ACADEMIC. KARIBU SANA
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. GetInformedTz - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger